Tuesday, July 19, 2016

*BALOZI IDDI AMKABIDHI RIPOTI MIRADI YA UPANUZI WA UWANJA WA NDEGE WA ZANZIBAR BALOZI WA CHINA NCHINI TANZANIA

 Balozi wa China, Lu Youqing akipokea Ripoti aliyoiomba  kutoka kwa Balozi Seif Ali Iddi inayofafanua kwa kina mikataba ya miradi ya upanuzi wa sehemu ya Maegesho ya Ndege kwenye uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Zanzibar ili kusaidia ukamilishaji wa miradi hiyo. Makabidhiano ya Ripoti hiyo yamefanyika Nyumbani kwa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Bara bara ya Haile Sellasie Jijini Dar es salaam.
 Balozi wa Jamuhuri ya Watu wa China, Lu Youqing aliyepo kati kati akimueleza Balozi  Seif ujio wa Ujumbe wa ngazi ya Juu ya Benki ya Kimataifa ya China ya Exim kwa lengo la kukagua miradi inaqyofadhiliwa na Taasisi hiyo ya Kifedha.
Makamu wa Pili w Rais wa Zanzibar Balozi Seoif (kushoto) akibadilishana mawazo na Balozi wa China Nchini Tanzania, Lu Youqing aliyepo kati kati baada ya kukamilisha mazungumzo yao Jijini Dar es salaam.  Picha na – OMPR – ZNZ.
********************************************************
Ujumbe wa Benki ya Kimataifa ya Jamuhuri ya Watu wa China ya Exim
Bank ukiongozwa na Mkuu wa Benki hiyo unatarajiwa kuwasili Zanzibar
mnamo Tarehe 21 Mwezi huu wa Saba kwa ziara rasmi ya kutembelea miradi
inayofadhiliwa na Taasisi hiyo ya Kifedha ya Nchini China.
Balozi wa Jamuhuri ya Watu wa China Nchini Tanzania Bwana Lu Youqing
alitoa kauli hiyo wakati wa mazungumzo yake Nyumbani kwa Makamu wa
Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Bara Bara ya Haile
Selassie Jijini Dar es salaam kufuatia muendelezo wa mazungumzo yao
kuhusu miradi inayofadhiliwa na Serikali ya China kupitia Benki ya
Exim.
Mazungumzo hayo yamekwenda sambamba na Balozi wa China Bwana Lu
Youqing kupokea Ripoti aliyoiomba kutoka kwa Balozi Seif Ali Iddi
inayofafanua kwa kina mikataba ya miradi ya upanuzi wa sehemu ya
Maegesho ya Ndege kwenye uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Zanzibar ili
kusaidia ukamilishaji wa miradi hiyo.
Balozi Lu Youqing alisema ujumbe huo wa Benki ya Exim utatembelea na
kuona maendeleo ya ukamilishaji wa ujenzi wa sehemju ya Maegesho ya
Ndege katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Amaani Abeid Karume
Kisauni pamoja na kukagua eneo la Mpiga duri linalotarajiwa kujengwa
Bandari ya Kimataifa ya upakizi na ushushaji wa Mizigo.
Balozi Lu alifahamisha kwamba pamoja na ziara hiyo ujumbe huo pia
utafanya mazungumzo ya pamoja na Mawaziri wanaosimamia Wizara za Fedha
na Mipango na Ujenzi, Miundombinu na Mawasiliano na watendani
waandamizi katika jitihada za kuongeza nguvu za kukamilisha miradi
hiyo.
Alisema ripoti aliyoipokea kutoka kwa Balozi Seif itamrahisishia kazi
yake ya ufuatiliaji wa muendelezo wa miradi hiyo na kuelezea faraja
yake kwamba uhusiano kati ya Jamuhuri ya Watu wa China na Zanzibar
utaendelea kuimarika zaidi kwa karne nyingi ijayo.
Akitoa shukrani zake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif
Ali Iddi alisema Zanzibar inaendelea kuthamini hatua zinazochukuliwa
na Jamuhuri ya Watu wa China kupitia Benki yake katika kufadhili
miradi mbali mbali ya Maendeleo na Uchumi Visiwani Zanzibar.
Balozi Seif alisema Jamuhuri ya Watu wa China imeonyesha wazi kuguswa
kwake na harakati za kimaendeleo zinazochukuliwa na Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar katika kuwajengea miundo mbinu imara Wananchi
wake kwenye sekta tofauti zitakazosaidia kuwakwamua kutokana na ukali
wa maisha.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif ameipongeza Serikali ya
Jamuhuri ya Watu wa China kupitia Balozi zake za Zanzibar na Tanzania
kwa ujumla katika kuunga mkono miradi ya Maendeleo ya Wananchi wa
Zanzibar.
Balozi Seif Ali Iddi yupo nyumbani kwake Dar es salaam kwa mapumziko
mafupi akiwa njiani kujiandaa kuelekea Mjini Dodoma kuhudhuria vikao
vya juu vya Chama cha Mapinduzi ukiwemo Mkutano Mkuu Maalum wa CCM wa
kumkabidhi Uwenyekiti Rais wa sasa Dr. John Pombe Magufuli.

No comments:

Post a Comment