Saturday, March 29, 2014

*BUNGE MAALUM LA KATIBA LAPITISHA AZIMIO LA KURA YA MSETO



Hatimaye baada ya mvutano wa baadhi wa wajumbe wa Bunge la  Maalum la Katiba kuhusu upigaji wa kura ya siri na ya wazi kuendelea  leo  Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge Maalum, Mhe . Pandu Ameir Kificho amewasilisha  azimio la mapendekezo ya  ya upigaji kura wa wazi na siri  kutumika kwa pamoja katika kaununi ya 37 na 38, ambalo limetipitishwa na Bunge hilo kwa  matokeo ya  jumla kwa kura  ya ndiyo 376 na hapana 133 .

Kura hizo zimetangazwa na Makamu Mwenyekiti wa Bunge ,hilo, Mhe.Samia  Sululu kabla ya kuahirisha  kikao hicho leo usiku, ambapo  alisema   azimio hilo limepitishwa na Bunge hilo , kufuatia  upigaji wa kura ,ambapo  idadi ya kura zilizopigwa ni  509, wakati mauhudhurio  ya wajumbe yalikuwa 511.
Mhe . Samia alisema kwa  upande wa kura za wazi zilizopigwa ni 438, ambazo za ndiyo zilikuwa 351 na hapana ni 87, wakati kura za siri  zilizopigwa zilikuwa ni 71, ambazo  za ndiyo zilikuwa 25 na hapana ni 46.

Uamuzi huo umefuatiwa  baada  ya hali hiyo ambayo ilitokea tena  kwa mara nyingine jana jioni  mara baada ya Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge Maalum, Mhe . Kificho kuwasilisha mapendekezo  ya upigaji kura wa wazi na siri  kutumika kwa pamoja katika kaununi  hizo.

Tangu jana jioni na leo  baadhi ya wajumbe wamekuwa wakitoa michango kutaka upigaji kura huo uwe wa wazi  na siri , huku wengine kutaka kura ya siri.
Awali  Kanuni za 37 na  38 zilibaki kiporo tangu wakati wa utungaji wa kanuni   mbalimbali za Bunge hilo,  na uchangiaji wa kuziboresha, kutokana na mvutano huo, ambao baadhi ya wajumbe  kutaka kura ya uwazi na wengine siri.
Wakizungumzia juu ya makubaliano yaliyofanywa na Kamati ndogo ya Muda ya Maridhiano  na Kamati ya  Kanuni na Haki za Bunge  kuhusu mapendekezo ya upigaji kura huo.  
Mmoja ya wajumbe wa Kamati hiyo ndogo ya Maridhiano, John Nyika alisema  walifanya mazungumzo hayo waliona ni vema  wakubaliana   mtu anayeweza kupiga kura ya uwazi  na anayetaka ya siri wapige kulingana na matakwa yao  ili kuwezesha mchakato huo kupiga hatua mbele.

“ Tunaomba utaratibu huu wa maridhiano  uendelee  … ili tuweze kupiga  hatua  mbele,” huku akisisitiza hawana dhamira yoyote ya  kukwamisha mchakato wa Katiba mpya. Hivyo watakuwa wa kwanza kuunga mkono kwa kura azimio litakalopitishwa kwa kura zitakazokubaliwa.
Naye mjumbe mwingine wa kamati hiyo , Vuai Ali Vuai alisema jambo hilo ni kubwa  kwa Watanzania ndio maana wanatakiwa kupiga kura kwa uwazi umma uweze kuona .

 Kwa upande wake ,mjumbe mwingine wa kamati hiyo ya ndogo  ya Maridhiano Askofu Mkuu Mstaafu wa Kanisa la Anglikana Tanzania, Donald Mtetemela amesema   ni vizuri wajumbe hao wakakubali azimio hilo kwa kuwa mpaka sasa wameshatumia siku 40 kujadili kanuni za kuongoza Bunge hilo na zimetumia gharama hivyo wasiendelee kuongeza gharama, zipo siku tatu za kuomba ili kufanikisha maridhiano hayo.

“ Ninawaomba wajumbe wenzangu kukubali azimio hili ili tuweze kusonga mbele na na mchakato wa kupata Katiba ,” alisema Askofu Mtetemela

No comments:

Post a Comment