Saturday, March 29, 2014

*WIZARA YA HABARI, VIJANA, UTAMADUNI NA MICHEZO KUANDAA KONGAMANO



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo yenye jukumu la kusimamia sekta ya Vijana nchini imeandaa Kongamano la Vijana kutoka Vyuo vya Elimu ya Juu kuhusu Wajibu wa Vijana katika Kuimarisha Muungano Wetu Miaka 50 tangu kuzaliwa kwake. 

Kongamano hili la Vijana kuhusu Muungano linafanyika Jumapili Machi 30, 2014  kuanzia Saa  5:00 Asubuhi katika ukumbi wa Ubungo Plaza, Dar es Salaam na litarushwa moja kwa moja na Televisheni ya Taifa, TBC One na TBC Taifa.

Kongamano hili ni sehemu ya sherehe za miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar tangu kuasisiwa kwake na Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Mzee Abeid Aman Karume aliyekuwa Rais wa Kwanza wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Aprili 26, 1964.

Kauli mbiu ya sherehe za Miaka 50 ya Muungano ni “UTANZANIA WETU NI MUUNGANO WETU, TUULINDE, TUUIMARISHE NA KUUDUMISHA”.


Lengo la Kongamano hili ni kuzungumzia Wajibu wa Vijana katika kuimarisha Muungano ambao mwezi  ujao unafikisha miaka 50.Washiriki wa Kongamano hili  ni vijana  300 kutoka Vyuo vya Elimu ya Juu vilivyopo Tanzania Bara na Zanzibar.

Washiriki wa Kongamano hili watapata fursa ya kuwasikia watoa mada ambao ni Wahadhiri wa Vyuo Vikuu Prof. Gaudens Mpangala atakayewasilisha mada kuhusu Wajibu wa Vijana katika Kuimarisha Muungano, Miaka 50 tangu kuzaliwa kwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar. Aidha mada kuhusu Mapendekezo ya Katiba Mpya kwa Mustakabali wa Muungano wetu itawasilishwa na Prof. Issa Shivji.

Waandishi wa Habari kutoka Vyombo mbali mbali vya Habari nchini wanakaribishwa kushiriki kwa lengo la kuhabarisha umma kuhusu kongamano hili.

Imetolewa na Idara ya Habari -  MAELEZO
29 Machi 2014

No comments:

Post a Comment