Friday, June 21, 2013

*TANSEED KUDHIBITI MAGUGU HATARI YA KIDUHA


KAMPUNI ya mbegu ya TANSEED International yenye makao makuu mjini Morogoro imeandaa maonesho ya shamba darasa ya teknolojia mpya ya mbegu za mahindi ya TAN 222 kukomesha kiduha “trigaway maize”kwa ajili ya kudhibiti magugu hatari ya kiduha kwenye zao la mahindi. 

Maonesho hayo yatafanyika  kesho (Jumamosi)  katika maadhimisho ya siku ya wakulima (Farmer Field Day) katika kijiji cha Mkuza  wilayani Mheza ambapo Mgeni Rasmi atakuwa Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Chiku Galawa.

Ambapo  yatahudhuriwa na watafiti wa mazao ya kilimo, wataalamu wa ugani, makampuni ya mbegu, wakulima, taasisi za serikali  na zisizo za kiserikali mkoani humo. 

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Isaka Mashuri leo jijini Dar es salaam  katika ukumbi wa mikutano wa Idara ya Habari -MAELEZO alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari juu ya maadhimisho hayo yatakayofanyika mkoani Tanga.

Alisema lengo la maonesho hayo ni kuhamasisha wakulima, watafiti, washauri wa ugani, wasiasa, taasisi za serikali na zisizo za kiserikali  pamoja na wadau wengine ni kuhusu tishio linatokana na magugu ya kiduha.
“Magugu ya kiduha yamekuwa ni tatizo kubwa kwa wakulima wa nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara kwa kipindi cha miongo saba. Kiduha ni magugu tegemezi yanayojishikiza kwenye mizizi ya mazao ya nafaka  na kunyonya maji , madini na virutubisho vingine.” alisema  Mashuri.

Mashuri aliongeza  kuwa magugu hayo huharibu ya mahindi kwa kutoa sumu na kuweza kuangamiza mimea ya mazao hata kabla magugu hayajajitokeza juu ya ardhi. 

“Magugu ya kiduha huzaa mbegu nyingi kati ya 5,000 hadi 200,000 kwa mmea mmoja, hivyo kufanya tatizo kuwa kubwa zaidi kwani mbegu za kuduha huweza kubaki zikiwa hai  aridhini kwa muda mrefu zaidi ya miaka 20 na zaidi na kusababisha upungufu wa chakula kila mwaka, ” alisema  Mashuri. 

Alisema kwamba inakadiriwa kuwa takribani hekari milioni 1.5 za ardhi Afrika Mashariki zimeathiriwa na magugu ya kiduha ambapo  aliitaja mikoa iliyoathirika Tanzania  na magugu  hayo ni pamoja na Morogoro, Pwani , Tanga, Dodoma,Singida, Tabora, Shinyanga , Mwanza, Mara, Ruvuma, Iringa, Mbeya, Rukwa, Lindi  na  Mtwara na kubainisha kuwa ni zaidi ya ekari 1,500,000 zimeathirika.

Aidha  Mashauri alieleza  kuwa magugu hayo husababisha upotevu wa mavuno takribani tani  milioni 1.7 za nafaka zenye thamani ya Dola za Kimarekani milioni 356 ambazo ni sawa na Sh.bilioni 584.6 za Kitanzania kwa mwaka.

Naye Mkurugenzi wa Shirika la BASF Nchini Kenya linalojishughulisha na shughuli za madawa ya kilimo, Sammy Wairuingi alisema kuwa Tanzania tushangilie kwa furaha ya kuja kwa fursa hii ya teknolojia mpya kwani itasaidia kuzalisha chakula cha kutosha kulisha familia ,kufukuza njaa na umasikini.

Kampuni ya TANSEED inashirikiana na Taasisi ya Kimataifa ya Utafiti wa Mahindi na Ngano ‘ International Maize and Wheat Improvement Centre’ (CIMMYT),  Taasisi ya kimataifa ya ‘African Agriculture Technology Foundation’ (AATF) inayojishughulisha na kuunganisha sekta za umma na binafsi katika usambazaji wa teknolojia za kilimo, na kampuni ya madawa ya kilimo na majumbani BASF

No comments:

Post a Comment